MASOMO YA MISA 14/06/2025

JUMAMOSI JUMA 10 LA MWAKA WA 1

MASOMO

SOMO 1:
 2.Kor.5:14–21
Upendo wa Kristo watubidisha; maana tumehukumu hivi, ya kwamba mmoja alikufa kwa ajili ya wote, basi walikufa wote; tena alikufa kwa ajili ya wote, ili walio hai wasiwe hai tena kwa ajili ya nafsi zao wenyewe, bali kwa ajili yake yeye aliyekufa kwa ajili yao. Hata imekuwa, sisi tangu sasa hatumjui mtu awaye yote kwa jinsi ya mwili, lakini sasa hatumtambui hivi tena. Hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita; tazama! Yamekuwa mapya. Lakini vyote pia vyatokana na Mungu, aliyetupatanisha sisi na nafsi yake kwa Kristo amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita; tazama! Yamekuwa mapya. Lakini vyote pia vyatokana na Mungu, aliyetupatanisha sisi na nafsi yake kwa Kristo, naye alitupa huduma ya upatanisho; yaani, Mungu alikuwa ndani ya Kristo, akiupatanisha ulimwengu na nafsi yake, asiwahesabie makosa yao; naye ametia ndani yetu neno la upatanisho. Basi tu wajumbe kwa ajili ya Kristo, kana kwamba Mungu anasihi kwa vinywa vyetu; twawaomba ninyi kwa ajili ya Kristo mpatanishwe na Mungu. Yeye asiyejua dhambi alimfanya kuwa dhambi kwa ajili yetu, ili tupate kuwa haki ya Mungu katika Yeye.

WIMBO WA KATIKATI: Zab.103:1–4,8–9,11–12 (K)8
1. Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana.
Naam, vyote vilivyo ndani yangu
Vilihimidi jina lake takatifu.
Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana,
Wala usizisahau fadhili zake zote.

(K) Bwana hatateta siku zote.

2. Akusamehe maovu yako yote,
Akuponya magonjwa yako yote.
Aukomboa uhai wako na kaburi,
Akutia taji ya fadhili na rehema. (K)

3. Yeye hatateta siku zote,
Wala hatashika hasira yake milele.
Hakututenda sawasawa na hatia zetu,
Wala hakutulipa kwa kadiri ya maovu yetu. (K)

4. Maana mbingu zilivyoinuka juu ya nchi,
Kadiri ileile rehema zake ni kuu kwa wamchao.
Kama mashariki ilivyo mbali na magharibi,
Ndivyo alivyoweka dhambi zetu mbali nasi. (K)


SHANGILIO: Yak 1:18
Aleluya, aleluya!
Kwa kupenda kwake mwenyewe,
Baba alituzaa sisi kwa neno la kweli,
tuwe kama limbuko la viumbe vyake.
Aleluya!

INJILI: 
Mt.5:33-37
Tena mmesikia watu wa kale walivyoambiwa: Usizini, ila mtimizie Bwana nyapo zako; lakini mimi nawaambia: Usiape kabisa; hata kwa mbingu, kwa maana ndicho kiti cha enzi cha Mungu; wala kwa nchi, kwa maana ndiyo pa kuwekea miguu yake; wala kwa Yerusalemu, kwa maana ndio mji wa Mfalme mkuu. Wala usiape kwa kichwa chako, maana huwezi kufanya unywele mmoja kuwa mweupe au mweusi. Bali maneno yenu yawe Ndiyo, ndiyo; Siyo, siyo; kwa kuwa yazidiyo hayo yatoka kwa yule mwovu.

MAOMBI
Ndugu, kwa maombezi ya Bikira Maria, tumwombe Mungu aliyemfanya Yesu Kristo, asiyejua dhambi kuwa dhambi kwa ajili yetu.

Kiitikio: Upokee ombi letu.
1. Upendo wa Kristo uwabidishe viongozi wa Kanisa kujitoa kabisa kwa ajili ya huduma kwa wote. Ee Bwana.

2. Uwajalie mataifa yote mapatano na mshikamano wenye kuwanufaisha watu wako kimwili na kiroho. Ee Bwana.

3. Wote wanaoitwa kwa kazi za kitume wawe tayari kuacha yote, kukufuata bila masharti na kuwahudumia walengwa bila ubaguzi. Ee Bwana.

4. Umpe kila mmoja wetu neema ya uaminifu katika kuyatimiza yale uliyotuagiza kufanya kadiri ya hali yetu ya maisha. Ee Bwana.

5. Wewe unayetia ndani yetu neno la upatanisho, uwasamehe marehemu wetu dhambi zao, wapate kuishi nawe milele mbinguni. Ee Bwana.

Ee Mungu uliyemchagua Bikira Maria awe mwombezi wetu, uyapokee maombi yetu. Kwa njia ya Kristo Bwana wetu. Amina.



No comments

Post a Comment

Shajara Yetu © all rights reserved
MKATOIKI KIGANJANI by mitume technologies